Sunday, June 2, 2013

ADDIS ABABA: TAIFA STARS, SUDAN SARE!

STARS KUONDOKA ETHIOPIA LEO, KUPITIA CAIRO KWENDA MOROCCO!
 
PATA HABARI KAMILI: 

Release No. 094

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Juni 2, 2013

TAIFA_STARS-FRAMEDTAIFA STARS, SUDAN ZATOKA SULUHU
Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) imetoka sare ya bila kufungana na Sudan (Nile Crodcodile) katika mechi ya kujipima nguvu iliyochezwa leo (Juni 2 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Addis Ababa nchini Ethiopia.

Mechi hiyo iliyochezeshwa na mwamuzi Bamlak Tessema wa Ethiopia ilikuwa sehemu ya maandalizi kwa timu zote ambazo wikiendi ijayo zinacheza mechi za mchujo za Kombe la Dunia. Wakati Stars itakuwa ugenini nchini Morocco, Sudan itacheza nyumbani dhidi ya Ghana.

Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager ilicheza vizuri mechi hiyo, hasa kipindi cha pili ambapo ilifanikiwa kutengeneza nafasi kadhaa za kufunga lakini ama washambuliaji walipiga nje au mipira yao kuokolewa na kipa Ehab Abdelfatahh wa Sudan.

Washambualiji wa Stars akina Khamis Mcha, Mrisho Ngasa na Amri Kiemba wakiongozwa na John Bocco walilitia msukosuko mara kwa mara lango la Sudan ambalo lilikuwa chini ya beki wa kati Nadir Eltayeb ambaye alifanya kazi ya ziada dakika ya 72 kuokoa mpira uliokuwa ukielekea wavuni.

Stars katika mechi hiyo iliwakilishwa na Juma Kaseja, Nadir Haroub/Vicent Barnabas, Shomari Kapombe, Kelvin Yondani, Aggrey Morris, Frank Domayo, Mrisho Ngasa, Salum Abubakar, John Bocco/Haruni Chanongo, Amri Kiemba/Khamis Mcha na Simon Msuva/Athuman Idd.

Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia, Joram Biswaro amewataka wachezaji wa Taifa Stars kuhakikisha wanaipeleka timu hiyo kwenye fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika mwakani nchini Brazil.

Timu inaondoka kesho alfajiri kwenda Morocco kwa kupitia Cairo, Misri ambapo inatarajia kuwasili Casablanca saa 8 mchana.

Boniface Wambura

Ofisa Habari

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Addis Ababa

No comments:

Post a Comment